Jumanne, 3 Januari 2017

KATIBU TAWALA MKOA WA SONGWE ATOA SOMO KWA WATUMISHI WA UMMA MKOANI SONGWE

Na Daniel Mwambene Songwe                           
Watumishi wa umma mkoani Songwe  wametakiwa kutulia katika vituo vyao vya kazi ili kuwatumikia wananchi na kuwapunguzia gharama za kuendesha familia zao.

Wito huo ulitolewa na Katibu Tawala wa Mkoa wa Songwe Mh. Elia Tandu wakati alipokuwa akizungumza na Wakuu wa Idara na vitengo katika  Halmashauri ya Wilaya ya Ileje kwenye ukumbi wa Mkuu wa Wilaya hiyo akiwa katika ziara ya kikazi.

Mh. Tandu alisema kuwa kutotulia katika vituo vya kazi siku za mwisho wa juma kwa baadhi ya watumishi hao kwa kisingizio cha kusafiri kwenda kuona familia zao kuna athari kubwa kwa serikali,wananchi na kwa maisha ya mtumishi mwenyewe.

Alisema kuwa limekuwa tatizo kubwa kwa baadhi ya watumishi wa umma kusafiri nje ya wilaya zao na mkoa siku za mwisho wa juma na sikukuu bila kufuata taratibu za kisheria hali inayosababisha usumbufu kwa waajiri wao pindi wanapowahitaji katika kipindi hiki cha serikali ya Awamu ya Tano yenye kauli mbiu “Hapa Kazi tu”.

Aliongeza kuwa huduma kwa wananchi zinategemea sana uwepo wao wa karibu hivyo kukosekana kwao kunawaongezea wananchi ugumu wa maisha.

Pia aliwaambia watumishi hao kuwa, kuwa mbali na familia zao kwa kisingizio cha mazingira magumu ya vituo vya kazi kunawaongezea gharama za maisha ambazo hazina msingi wowote kwakuwa wanakuwa na bajeti za familia mbili kwa wakati mmoja sawa na mwanaume mwenye mitala (wake wawili).

Alisema kuwa kupangiwa katika maeneo hayo hawana budi kujua kuwa wana jukumu la kuzibadilisha jamii wanazozikuta badala ya kuendelea kulalamikia ugumu wa mazingira huku wao wakitakiwa kuwasaidia wananchi kuwa chachu ya maendeleo.

Akifafanua zaidi alisema kuwa mkoa wilaya nyingi za mkoa wa Songwe zina changamoto zinazotautiana hivyo serikali iliwatuma kutumia taaluma zao kwa kusaidiana na wananchi kuzikabiri changamoto hizo.

Aliongeza kuwa kwa mtumishi yeyete kuwa na fikra za kuhama huwa kunamchelewesha kimaisha hali aliyoielezea kuwa haina budi kuachwa kwa kuwa wamejikuta hawahami huku wakiwa wametumia rasilimali nyingi katika kutafuta uhamisho huo.

Alisema kuwa kwa mtumishi yeyote ili kulinda utulivu wa akili yake hana budi kukifanya kituo chake cha kazi kuwa ni makazi yake ya kudumu hali itakayomwongezea ubunifu katika mambo anayoyafanya kila siku.

Akizungumza na watumishi wa kada mbalimbali katika wa halmashauri hiyo kwenye Ukumbi wa Mwala mjini Itumba Katibu Tawala huyo aliwataka watumishi hao kuzingatia maadli ya utumishi wa umma nakuepukana na vitendo vyote vinavyoweza kupunguza kasi ya utendaji wa serikali ya awamu hii yenye kupigania maslahi ya wanyonge.

Alisema kuwa mshikamano baina ya watumishi wa idara mbalimbali ni silaha itakayoupeleka mkoa wa Songwe mahali panapotakiwa na taifa letu lenye kuijenga Tanzania ya viwanda.
Aliwataka watumishi wa mkoa wa Songwe kuwa wavumilivu katika kipindi hiki cha mpito ambapo serikali inashughulikia uhalali wa watumishi wa umma kwa kuondoa watumishi hewa na wenye vyeti vya bandia (feki).

Kwa upande wao watumishi hao waliomba serikali iharakishe mazoezi ya uhakiki wa watumishi ili wale wanaotaka kuhama kwasababu za msingi waweze kufanya hivyo.
  
 Katibu Tawala wa Mkoa wa Songwe Mh.Elia Tandu (kushoto) akisalimiana na Mkuu wa Wilaya ya Ileje Mh. Joseph Mkude (kulia) alipowasili ofisi za wilaya hiyo

 Mh. Elia Tandu akizungumza na watumishi kwenye Ukumbi wa Mwala uliopo shule ya sekondari ya Itumba
Watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ileje wakimsikiliza Katibu Tawala wa Mkoa wa Songwe kweny Ukumbi wa Mwala

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni