Jumatatu, 9 Januari 2017

SERIKALI WILAYANI ILEJE YAHIMIZA UJENZI WA VYOO BORA

Wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama wakielekea kukagua choo cha wanafunzi shule ya sekondari Nakalulu

Mkuu wa Wilaya ya Ileje Mh. Joseph Mkude amewagiza viongozi wa Serikali za Mitaa wilayani humo kuhakikisha wanasimamia vyema ujenzi wa vyoo bora katika shule na kuondokana na ujenzi wa vyoo vya muda.

Alitoa maagizo hayo wakati akiongoza Kamati ya Ulinzi na Usalama kukagua shughuli za ujenzi katika baadhi ya shule za sekondari ikiwa ni siku moja kabla ya kuanza muhula wa kwanza wa masomo 2017.

Ziara hiyo ililenga katika kujiridhisha na maandalizi ya uwepo na ubora wa vyoo,vyumba vya madarasa na matumizi sahihi ya fedha zinazotolewa na serikali.

Mh.Mkude akizungumza kwa nyakati tofauti katika shule za sekondari Itumba,Ileje,Nakalulu Kakoma na Mbebe alisikitishwa na hali aliyoiona katika baadhi ya shule hizo katika vyoo vya walimu na wanafunzi akisema kuwa haviendani na hadhi ya walimu.

Alisema kuwa vyoo vilivyopo katika shule za Nakalulu na Kakoma havichochei walimu kupenda mazingira ya kazi na haviendani na viwango vyao vya elimu ambayo ni mwanga kwa jamii inayozunguka shule.

‘’Vyoo vya shule vikiwa bora vinaweza kubadilisha ubora wa vyoo katika jamii kwa vile wanafunzi wakihitimu wataiga ujenzi huo na kuboresha zaidi na kabla ya mtu kuanza na ujenzi ya nyumba ya kuishi choo kiwe cha kwanza’’,alisema Mh. Mkude.

Akizungumza katika sekondari ya Mbebe aliwataka madiwani kuwatumia vema wataalam waliopo katika halmashauri hiyo kwenye masuala ya ujenzi na manunuzi ili kuijengea heshima halmashauri hiyo.

Kauli hiyo pia ilifuatia kasoro alizozibaini kwenye manunuzi ya mabati ya shule ya sekondari ya hiyo ambapo mabati 115 yalibainika kuwa chini ya viwango vinavyotakiwa katika majengo ya serikali hali iliyosababisha aagize yarudishwe kwa mwuzaji na kuchukua mabati yanayotakiwa.

Kwa upande wao, viongozi wa Halmashauri ya Wilaya hiyo walipongeza juhudi zinazofanywa na kiongozi huyo,katika usimamizi wa shughuli za maendeleo kwa kufika maeneo husika bila kusubiri taarifa za mezani wakisema watendaji wengine hawana budi kuunga mkono juhudi hizo.

Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, alimfananisha kiongozi huyo na baadhi ya viongozi waliotangulia ambao ni aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo marehemu Stivin Kibona, aliyekuwa Mkuu wa Wilaya hiyo marehemu Luhonzyo Siwale pamoja marehemu Mwangomo aliyekuwa Afisa Maliasili ambao alisema licha ya kuondoka hapa duniani bado matunda ya kazi zao yanaonekana.

Naye Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya hiyo Mh.Gwalusako Kapesa alimpongeza Mkuu wa Wilaya kwa jinsi anavyokuwa wazi hali aliyoielezea kuwa inaashiria ucha Mungu na ikifanywa na viongozi wengine itajenga hali kuaminiana katika kazi.

Pamoja na mambo mengine Mkuu wa Wilaya aliwataka viongozi wote kushirikiana katika kuhakikisha wanafunzi wote waliochaguliwa kuanza kidato cha kwanza wanafanya hivyo na kufuatilia kwa kina wale wanaosena wamekwenda shule za binafsi badala ya zile za serikali.

Huku hali ikiwa mbaya kwa shule hizo kwa upnde wa vyoo bado kuna shule zimenufaika na ujenzi wa vyoo bora kwa ufadhili wa SEDP ambazo ni Luswisi,Itale,Msomba na Bupigu.
Vyoo vya walimu na wanafunzi katika sekondari ya Kakoma kilichojengwa chini ya viwango ambacho Mkuu wa Wilaya alikelezea kuwa kinadhalilisha watumishi wa Umma


 Mkuu wa Wilaya ya Ileje (kulia) akipata maelezo toka kwa Afisa Mtendaji wa kata ya Mbebe Nickson Mwashitete (kushoto) kuhusu matumizi ya fedha zilizotolewa na Halmashauri kwa shule ya sekondari Mbebe
 Mh.Mkude akiangalia ubora wa mabati kulingana na viwango vinavyotakiwa na serikali ambapo akisaidiwa na Mhandisi wa Ujenzi wa Wilaya alibaini mabati 115 yasiyokidhi viwango katika sekondari ya Mbebe.
 Wajumbe wa Kamati ya Ulinzina Usalama wakikagua jengo mojawapo katika sekondari ya Mbebe
Wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama na viongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ileje wakimsikiliza Mkuu Wilaya (hayupo pichani) ni ndani ya chumba cha darasa katika sekondari ya Mbebe.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni