Jumapili, 1 Januari 2017

SALAMU ZA MWAKA MPYA TOKA KWA Mh. JOSEPH MODEST MKUDE MKUU WA WILAYA YA ILEJE

SALAMU ZA MWAKA MPYA 2017 TOKA KWA MHESHIMIWA JOSEPH MODEST MKUDE (MKUU WA WILAYA YA ILEJE)  
Ndugu Wananchi wote wa Wilaya ya Ileje tunapoelekea kumaliza Mwaka 2016 na kuukaribisha Mwaka mpya 2017, napenda kutumia nafasi hii kutoa salamu za Mwaka mpya natoa pole kwa maafa yaliyotokea katika Kata ya Mbebe.
Tarehe 21/12/2016 mnamo saa 9.02 alasiri kulitokea maafa hayo yaliyosababishwa na mvua iliyoambatana na upepo mkali katika Vijiji vya Mbebe, Mapogoro na Shinji
Madhara yaliyotokea ni  pamoja na:-
·         Kifo cha mtoto wa miezi- 6
·         Kujeruhiwa kwa watu- 21
·         Kaya 162 kuezuliwa nyumba zao
·         Kuezuliwa kwa paa, madarasa mawaili shule ya msingi Mbebe na athari zilizotokea kanisa la Moravian, T.A.G, Sabato, Last church of god, Shinji United Church na Kanisa la Mizimu.
Kutokana na hali hiyo natoa pole sana kwa Wananchi wote waliopatwa na maafa hayo na  ninatoa wito kwa Ndugu, jamaa na marafiki na wadau wengine wote kuendelea kuwasaidia waathirika ili warudi katika maisha yao ya kawaida.
Aidha katika kipindi hiki kumetokea misiba na matatizo mbalimbali katika Wilaya yetu kwa mwaka huu 2016. Hivyo nawapa pole wote waliopatwa na matatizo mbalimbali.
Sambamba na hilo napenda kusisitiza mambo yafuatayo kwa Wananchi wote wa Ileje.
1.   Ujenzi wa nyumba bora
Katika ziara zangu Vijijini nimegundua kuwa nyumba nyingi zinajengwa bila kufuata viwango vinavyotakiwa kama vile kuweka rinta, kutumia miti au mbao ngumu na kutojenga misingi imara. Hivyo natoa wito kwenu kujitahidi kujenga nyumba kwa kufuata viwango vinavyotakiwa.

2.   Kupanda miti ili kuzuia upepo
Imebainika kuwa katika Wilaya yetu ya Ileje suala la upandaji miti na utunzaji mazingira kiujumla bado halijapewa uzito unaostahili. Miti inapandwa pale tu inapohitajika katika shughuli za kibiashara kama ilivyo katika kata za Ngulilo, Lubanda na Ibaba.

Si hivyo tu bali suala la upandaji miti ni muhimu sana katika utunzaji wa mazingira. Natoa wito kwenu wananchi katika msimu huu wa mvua kuendelea kupanda miti ya kibiashara kama tulivyozoea ambapo nawataka kila mtu kwenye kaya kupanda miti isiyopungua kumi (10) kwa kila mtu miti ikipandwa kuzunguka makazi yetu itasaidia sana kukinga upepo usiharibu makazi yetu.

Kwa taasisi kama vile shule za msingi na sekondari, makanisa, misikiti na sehemu nyingine za kazi hakikisheni mnapanda miti.

3.   Kilimo
Kufuatia utabiri wa hali ya hewa inayonyesha mvua zitakuwa za wastani na chini ya wastani,hivyo kuashiria kuwa mvua zitakuwa kidogo kwa uzalishaji.

Kwa mantiki hiyo, nasisitiza mnatakiwa kulima mazao yanayostahimili ukame kama vile mihogo na viazi vitamu.
·         Kutumia vizuri mlicho nacho ili kuepuka upungufu wa chakula kwene kaya zenu.
·         Kuendelea kufuata kanuni bora za kilimo na ushauri wa watalaam ili kuzalisha kwa tija.
·         Tumieni vema mabonde yenye unyevunyevu kwa kuzalisha mazao mbalimbali.

4.   Usafi wa mazingira
Napenda kuwakumbusha Wananchi juu ya umuhimu wa kuendelea kuzingatia usafi wa mazingira katika maeneo yetu. Serikali imetuagiza wote kushiriki kwenye usafi wa jumla kwa Nchi nzima siku ya kila jumamosi ya mwisho wa Mwezi, Na kwa Mkoa wetu wa Songwe tumeagizwa kila jumamosi kwa kila kaya kufanya usafi katika maeneo yake.

Nawashukuru wale wote wanajitokeza kufanya usafi katika maeneo yenu. Hata hivyo bado wapo Wananchi wachache ambao hawajitokezi kufanya usafi katika maeneo yao. Tayari nimetoa maelekezo kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya kuwa ahakikishe suala la usafi linatekelezwa kwenye Kata zote na kila mwisho wa Mwezi nipate taarifa ya utekelezaji wa usafi kwa Kata zote.

Pia viongozi wote ngazi ya Wilaya,Tarafa, Kata, Vijiji na Mitaa/Vitongoji wasimamie na kuhakikisha mitaa yao inakuwa safi. Usafi ni muhimu sana hasa wakati huu wa msimu wa mvua ili kuepuka magonjwa ya kuhara na pia kuondoa mazalio ya mbu.

5.   Hali ya usalama
Ndugu wanachi tuendelee kudumisha amani na utulivu katika Wilaya yetu. Hivyo ninatoa wito kwa yafuatayo ambayo yatakuwa ni endelevu katika kuendelea kudumisha amani tuliyonayo.
                        i.        Kuendelea kuwa na mahusiano mazuri kati yetu na Wilaya tunazopakana nazo. Ninatambua kwamba kuna baadhi ya maeneo ya mipaka ya Wilaya yetu na Wilaya jirani kuna migogoro ya ardhi ambayo tunaendelea kushughulikia na bila shaka yatapatiwa ufumbuzi haraka iwezekanavyo.
                       ii.        Kuendelea kuwa na mahusiano mazuri na Nchi jirani za Malawi na Zambia ambayo yapo kwa muda mrefu. Hivyo ninasisitiza ushirikiano huu uendelee na kuwa wa kimanufaa sio wa kiuharifu.
                      iii.        Kuendelea kushirikiana miongoni mwa kaya na kaya. Kwa kutoa taarifa mapema juu ya viashiria vya uvunjifu wa amani kwa raia.
                      iv.        Kuwa na ulinzi kati yetu wenyewe linapotokea au kabla ya kutoka jambo baya kutoa taarifa mapema kwa vyombo vya usalama.
                                   v.            Kujiepusha na vurugu zisizo na msingi kama vile uchomaji tairi barabarani, upigaji wa fataki, ulevi wa kupindukia n.k kwenye mkesha wa Mwaka mpya.

6.   Heri ya Mwaka mpya 2017
Natumia nafasi hii pia kuwatakia heri ya Mwaka mpya Wananchi wote wa Wilaya ya Ileje ili mwenyezi Mungu atusaidie tumalize salama Mwaka 2016 na tuuone Mwaka mpya wa 2017. Nawatakia wote Mwaka 2017 uwe ni wenye Baraka na mafanikio kwenu. Tusherekee kwa amani na utulivu sherehe za Mwaka mpya 2017.
Tunaposherekea Mwaka mpya ni vizuri Wananchi tukumbuke kuwa bado tunayo majukumu mbele yetu ya kuwaandaa na kuwapeleka watoto mashuleni hasa kwa wale wanaoenda kuanza kidato cha kwanza, Darasa la kwanza na Wanafunzi wengine ili mahudhurio ya Shule yawe mazuri kuanzia siku za mwanzo wa Mwaka. Maandalizi yafanyike mapema ili wanafunzi waripoti shuleni kwa tarehe iliyopangwa.

NAWATAKIA HERI YA MWAKA MPYA WA 2017.
MUNGU IBARIKI ILEJE
MUNGU IBARIKI SONGWE
MUNGU IBARIKI TANZANIA

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni